Mahakama ya Wilaya ya Ngorongoro leo tarehe 2 Februari, 2026 imeadhimisha siku ya Sheria nchini katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama ya Wilaya hiyo.

Maadhimisho hayo yamewakutanisha wananchi pamoja na wadau mbalimbali wakiwemo watumishi kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro na watumishi wa Mahakama hiyo, kwa lengo la kusherehekea siku hiyo muhimu katika mfumo wa utoaji haki nchini.
Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Mhe. Brigedia Jenerali Wilson Sakulo, amehudhuria maadhimisho hayo na kuungana na mgeni rasmi Mheshimiwa Bethsaida Steven Sivonike, Hakimu Mahakama ya Wilaya hiyo.
Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Mheshimiwa Sivonike alisema kuwa jukumu kuu la Mahakama ni kusikiliza mashauri na kutenda haki bila kujali hali ya mtu kijamii au kiuchumi, pamoja na kuhakikisha haki haitolewi kwa kuchelewa bila sababu za msingi.
Aliongeza kuwa Mahakama pia ina wajibu wa kutoa fidia stahiki kwa watu wanaoathirika kutokana na makosa ya watu wengine, kwa kuzingatia Sheria mahsusi zilizotungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

"Katika kutekeleza jukumu lake la utoaji haki, Mahakama inaongozwa na dira isemayo, haki sawa kwa wote, mapema na ipasavyo"-amesema Mhe. Sivonike

Hakimiliki©2017 NDC . Haki zote zimehifadhiwa.