Mwakilishi wa Mkurugenzi Bw. Lawrence Ledio, Maafisa lishe pamoja na wataalam mnamo tarehe 18 Aprili, 2024 waliambatana kwa pamoja kushuhudia zoezi la ufungwaji wa mashine ya kisasa ya kusaga unga wenye virutubisho vya Lishe katika kiwanda kidogo Cha kuzalisha unga wa mahindi Cha mfanyabiashara Ally Karanjai.
Mashine hiyo imefadhiliwa na Kampuni ya SANKU Mkoa wa Arusha. Mwakilishi kutoka kampuni ya Sanku Bw. Kelvin Urasa ametoa Elimu ya namna ya kufunga na kutumia mashine hiyo.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo Bw. Urasa ameeleza umuhimu wa kutumia mashine hiyo na faida ya matumizi ya unga wenye virutubisho kwa afya.
"Ni muhimu kutumia unga wa virutubisho wenye mchanganyiko wa madini ya Chuma, Zinki, Vitamini B 12 na Asidi ya Foliki"-Bw. Urasa
Naye mtaalamu wa Lishe Hospitali ya Wilaya ya Ngorongoro Bi. Angela Mbanga ametoa ufafanuzi na kuelezea faida ya unga wenye virutubisho kwa mtoto.
" Kutokana na virutubisho vilivyo katika unga husaidia kusafirisha hewa ya oksijeni kwenda kwenye ubongo, kutengeneza damu pia virutubisho hivi vinasaidia katika ukuaji wa mtoto na kuongeza nguvu kwenye misuli" Bi. Angela
Aidha Bi. Angela ameendelea kueleza umuhimu wa virutubisho hivi kwenye afya ya mtoto na kusema
"Virutubisho hivi ni muhimu na vitatusaidia sana kuboresha afya kwa Watoto wetu katika jamii zetu, hivyo ni muhimu kutoa virutubisho hivyo kwa Watoto mashuleni" ameongeza Bi. Angela
Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi Bw. Ledio ametoa shukrani kwa Meneja wa Kampuni ya SANKU kwa kuleta mashine hiyo Wilaya ya Ngorongoro.
"Tunashukuru kwa hatua hii ya awali kwani ndio mashine ya kwanza kufungwa katika Wilaya yetu, tumekua tukijadili kuhusu mashine za aina hii na leo tumeshuhudia ikifungwa tayari kwa ajili ya matumizi na itakwenda kusaidia kutoa huduma ya unga wa Lishe wenye virutubisho ili kupunguza udumavu kwa Watoto pamoja na matatizo kwa akinamama wajawazito." Bw. Ledio
Ikumbukwe suala la Lishe limepewa kipaumbele na Serikali ya awamu ya sita chini ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ili kuondoa hali ya udumavu kwa Watoto na kuboresha Afya ya Mama na mtoto.
https://www.instagram.com/p/C6Dep1UNAqs/?igsh=MXV5cDEydWdzeDZycQ==
Hakimiliki©2017 NDC . Haki zote zimehifadhiwa.