Mkutano wa robo ya Kwanza wa Baraza la madiwani Wilaya ya Ngorongoro umefanyika katika Ukumbi wa Mkutano wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro leo tarehe 12 Disemba, 2023. Kujadili agenda mbalimbali za kimaendeleo na ustawi katika Wilaya ya Ngorongoro.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro Mhe. Mohamed Bayo amesema Halmashauri imefanikiwa kutekeleza shughuli mbalimbali za kimaendeleo kutoka mwezi Julai Hadi mwezi Septemba, ambapo Halmashauri imekusanya mapato kutoka vyanzo mbalimbali jumla ya Tsh milioni 778,893,637, sawa na 25% hivyo kufikia makisio ya ukusanyaji fedha za mapato kwa Mwaka 2022,2023 na 2024.
"Katika hili hii ni hatua nzuri ya ukusanyaji wa mapato katika Halmashauri yetu hivyo tusibweteke, tuendelee na ukusanyaji na kukemea mianya ya upotevu wa mapato ili kufikisha huduma iliyokusudiwa kwa wananchi katika Wilaya yetu" amesema Mhe. Bayo
Aidha mwenyekiti amewapongeza madiwani pamoja na wataalamu mbalimbali katika wilaya ya Ngorongoro kwani Kasi ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo imeongezeka kwa kiwango kikubwa.
Sambamba na hayo Mwenyekiti ameipongeza Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro chini ya Bw. Nassoro B. Shemzigwa kwa kutoa msisitizo katika ukusanyaji wa marejesho ya mikopo kwa asilimia 10 ambapo imekusanywa takribani milioni 56, pia Mwenyekiti ametoa rai kwa wanaodaiwa mikopo kurejesha ili fedha hizo ziweze kufanyiwa maendeleo mbalimbali katika jamii.
Katika kuboresha sekta ya elimu na kusaidia wanafunzi kupata elimu katika mazingira mazuri, Halmashauri imefanikiwa kusajili shule mbili za msingi ikiwemo Losirwa iliyopo kijiji cha kirtalo na Katika kijiji cha Njorieti.
Hata hivyo Mhe. Bayo amewapongeza wataalamu wa elimu pamoja na walezi kwa kuongeza ufanisi katika ufundishaji kwa kuongeza ufaulu kutoka 60.7% kwa mwaka 2022 hadi asilimia 77.9 kwa mwaka 2023 sawa na ongezeko la asilimia 8.2 ,hivyo kutoka nafasi ya mwisho kimkoa na kushika nafasi ya tano.
Aidha Mwenyekiti ametoa muhtasari wa utelekelezaji wa Bajeti ya fedha kwa mwaka 2023 /2024 ambapo jumla kuu ya mapato ya ndani makisio yake ni Shilingi za Kitanzania 37,560,629,500. Huku jumla halisi ya mapato ya ndani ikiwa ni kiasi cha shilingi 15,230,529,837 za kitanzania hata hivyo kiasi cha Tsh milion 868,109,600 kutoka kwenye mapato kimetumika kwa matumizi ya ndani katika Wilaya ya Ngorongoro.
Ikumbukwe shughuli zote za maendeleo zinazofanyika katika Wilaya ya Ngorongoro ni utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya Mwaka 2020/2025 chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Hakimiliki©2017 NDC . Haki zote zimehifadhiwa.