Wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro wametakiwa kushiriki kikamilifu kufanya usafi wa mazingira na usafi binafsi ili kukabiliana na maambukizi ya ugonjwa wa trakoma.
Akizungumza katika kikao kazi cha kushughulikia magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele kilichofanyika leo April 14 katika ukumbi wa mikutano ya Domel mjini hapa, makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro ambaye pia ni Diwani wa kata ya Obalbal Mhe. Emanuel Tonge amesema ugonjwa wa trakoma unachangia pakubwa kuleta upofu kwa wananchi lakini hali hiyo kwasasa imepungua kutoka asilimia 15 kwa mwaka 2018 hadi asilimia 8.3 mwaka 2022 baada ya serikali kuanza zoezi la utoaji wa kinga na tiba ya ugonjwa huo.
Akizungumza kwa niaba ya Wizara ya Afya Dokta Ambakisye Mchiche ambaye ni Afisa ufuatiliaji wa mpango wa Taifa wa kukabiliana na magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele nchini, amesema juhudi zinahitajika ili kuiondoa Wilaya ya Ngorongoro katika kundi la Halmashauri tisa ambazo bado zina kiwango kikubwa cha maambukizi ya trakoma, pia ameongeza kuwa wilaya sabini bado zinapambana na trakoma huku wilaya zilizofanikiwa kutokomeza ugonjwa huo zikifikia sitini na saba.
Kwa upande wake mratibu wa magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele wilayani hapa Mwl.Emanuel Wilson Hamisi, amesema serikali ya wilaya ya Ngorongoro kupitia idara ya Afya inapanga kufanya zoezi la siku saba la ugawaji wa dawa za kinga na tiba dhidi ya ugonjwa wa trakoma kwa wananchi almaarufu vikope kuanzia tarehe 21 hadi 28 Aprili 2023 awamu ya kwanza na awamu ya pili kutekelezwa miezi mitano hadi 6 baadaye.
Ugonjwa wa trakoma ambao kitaalamu hujulikana kama Egyptian ophthalmia, ni ugonjwa unaosababishwa na bakteria waitwao klamidia trakomati na maambukizi yake husababibisha kukwaruza kwa sehemu ya ndani ya macho, mkwaruzo unaotajwa kusababisha maumivu ya macho, kuharibika kwa sehemu ya nje ya jicho na hatimaye upofu.
Hakimiliki©2017 NDC . Haki zote zimehifadhiwa.